Headlines News :

Monday, February 17, 2014

YAJUE MARADHI YA PUMU (ASTHMA) - 2



"Daktari nisaidie, nakufa mie" Wagonjwa wengi husema wanapoingia chumba cha daktari, wakiongea kwa taabu sana, huku wakipumua kwa taabu na mlio kama wa filimbi ukisikika. Madaktari huuliza maswali machache na kugundua ni PUMU.
PUMU ni ugonjwa sugu ambao huathiri njia ya hewa ambazo huingia na kutoa hewa katika mapafu. Upatapo ugonjwa wa pumu, kuta za ndani za njia ya hewa huvimba na hivyo kupunguza kiasi cha hewa kinachoingia na kutoka kwenye mapafu. Hali hii husababisha muathirika kutoa mlio kama wa filimbi au mluzi wakati wa kupumua, kifua kubana, kushindwa kupumua vizuri na kukohoa. Watu wenye pumu hupatwa na dalili hizi mara nyingi nyakati za usiku na asubuhi sana.
Kulingana na takwimu za hivi karibuni, huathiri watu milioni 300 duniani kote na zaidi ya milioni 22 wakiwa Marekani peke yake.
Ingawa ugonjwa huu huathiri watu wa rika zote, lakini mara nyingi huanza utotoni, huathiri watoto milioni 6 nchini Marekani. Ugonjwa wa pumu huua watu 255,000 duniani kote kila mwaka.
AINA ZA PUMU
PUMU YA UTOTONI (Child-Onset Asthma)
Hii ni aina ya pumu inayotokea baada ya mtoto kuwa kwenye vizio kama vumbi la wadudu mfano mende, manyoya ya wanyama wa kufugwa kama paka na mbwa. Pumu hii hutokea kwa kuwa mwili wa mtoto hutengeneza kingamwili (Antibodies) za IgE zinazosababisha pumu.
Ugonjwa wa pumu ni ugonjwa sugu uliopo sana kwa watoto waliozaliwa na uzito mdogo, wenye asili ya kiafrika, walio katika mazingira ya moshi pia waliolelewa latika mazingira ya dhiki/umaskini.
Watoto wengi huanza kuonyesha dalili wakikaribia miaka mitano. Huanza kama ugonjwa wa njia ya hewa kama mafua na kikohozi.
Watoto wa kiume wana hatari zaidi ya kupata pumu ikilinganishwa na watoto wa kike, ila hali hii huwa kinyume kipindi cha utu uzima.
Watafiti wanafikiri hali hizi huwapata watoto wa kiume zaidi kwa kuwa na njia za hewa nyembamba zaidi ikilinganishwa na njia za hewa za watoto wa kike. Hali hii hupelekea watoto wa kiume kuwa kwenye hatari zaidi wanapopatwa na maambukizi ya virusi mfano mafua.
PUMU YA UKUBWANI (Adult-Onset Asthma)
Pumu hii huanza baada ya kufika miaka 20. Pumu hii huathiri sana wanawake kuliko wanaume na pia haitokei sana kama pumu ya utotoni. Vizio pia husababisha aina hii ya pumu.
Inakadiriwa kuwa 50% ya pumu ya ukubwani husababishwa na vizio na aina hii ya pumu huitwa pumu ya ukubwani ya vizio ( Allergic adult-onset asthma). Na 50% haisababishwi na vizio (Allergens) nayo hujulikana kama pumu ya ukubwani isiyosababishwa na vizio (Non-allergic adult-onset asthma/Intrinsic asthma).
PUMU ITOKANAYO NA MAZOEZI (Exercise-induced asthma)
Ikiwa utakohoa na kukosa pumzi wakati wa mazoezi au baada ya mazoezi, inawezekana una pumu inayosababishwa na mazoezi. Ingawa kama sio mtu wa michezo kukimbia kwa kasi kwa angalau dakika 10 kunaweza kusanabisha kukosa pumzi na kukohoa. Ikiwa utakohoa na kukosa pumzi kwa muda mrefu basi hii itaonyesha una pumu inayosababishwa na michezo.
PUMU ITOKANAYO NA KUKOHOA (Cough-Induced Asthma)
Ni aina ngumu ya pumu kwa daktari kuweza kuigundua. Kwenye pumu hii inawezekana zisitokee dalili zingine zaidi ya kukohoa. Madaktari hulazimika kuchunguza sababu zingine za kukohoa sana na kuhakikisha sio zinazosababisha kukohoa huko.
PUMU ITOKANAYO NA KAZI (Occupational Asthma)
Aina hii ya pumu humtokea mtu akiwa mahali pake pa kazi. Huwatokea sana watumishi wa viwandani ambapo kuna kemikali, moshi na gesi (Nitrogen oxide) zinazoweza kuamsha pumu.
PUMU YA USIKU (Nocturnal Asthma)
Pumu hii hutokea kati ya saa 6 usiku na saa 2 asubuhi. Pumu hii huamshwa na vumbi, halufu kali kama za rangi ya nyumba na halufu ya vinyesi vya wanyama wa kufugwa. Mara nyingi wagonjwa hushtuka usingizini wakati wa usiku wa maanani baada ya kukosa pumzi.
PUMU KALI/PUMU ISIYOKUBALI STEROIDI (Severe Asthma/Steroidal-Resistant Asthma)
Wakati wagonjwa wengi wa pumu hupata nafuu baada ya matumizi ya steroidi, wachache hawapati nafuu. Hivyo wagonjwa hawa huhitaji matababu bora zaidi ya matibabu ya kawaida.
NINI HUSABABISHA PUMU?
Visababishi vya pumu havijulikani waziwazi, ingawa vitu vinavyoongeza hatari ya kupata pumu ni vizio mfano moshi, harufu, gesi na kemikali.
Kila mgonjwa wa pumu ana mzio. Zaidi ya 25% ya watu hupatwa na mafua yasababishwayo na mzio (Hay fever/Allergic rhinitis) na kuwashwa macho (Allergic conjuctivitis) pia wanaweza kupata pumu.
Mzio unaweza sababishwa na kingamwili (Antibodies) zilizo ndani ya damu zinazopelekea njia ya hewa kuvimba na kusababisha pumu.
Vizio vinasababisha sana pumu ni kama moshi, vumbi kutoka kwenye manyoya ya wanyama kama paka na mbwa, wadudu kama mende na halufu kali kama za manukato.
Moshi wa sigara unahusishwa sana na hatari ya kupata pumu pia hatari zaidi ya kufa kwa pumu. Watoto wa wazazi wanaovuta sigara wapo katika hatari ya kupata pumu. Pia watu wazima wanaovuta sigara wapo katika hatari ya kupata pumu.
Sababu zingine za kimazingira kama halufu (Marashi) inayosababishwa na vitu vya kusafishia nyumba pamoja na rangi za nyumba, hewa itokanayo na majiko ya gesi (Nitrogen oxide).
Uchafuzi wa mazingira kutokana na gesi (Sulfur dioxide, Nitrogen oxide) pia mazingira ya baridi huamsha ugonjwa wa pumu. Vitu hivi husababisha njia za hewa kusinyaa na kusababisha matatizo ya kupumua.
Watu wazima wenye uzito unaozidi kimo chao yaani wenye Body Mass Index (BMI) kati ya 25 na 30 wanaweza kupata pumu kwa 38% ikilinganishwa na watu wazima wenye uzito wa kawaida. Watu wanene zaidi wenye BMI ya 30 au zaidi wapo katika hatari mara mbili.
Watoto waliozaliwa kwa njia ya upasuaji wana hatari ya kupata pumu kwa 20% ikilinganishwa na watoto waliozaliwa kwa njia ya kawaida. Pia wajawazito wanaovuta sigara hupunguza utendaji wa mfumo wa hewa wa mtoto aliye tumboni hivyo huongeza hatari ya mtoto kupata pumu. Utafiti umeonyesha pia mtoto aliyezaliwa na uzito mdogo yupo kwenye hatari ya kupata pumu pia.
Watu walio na msongo wa mawazo (Stress) wapo katika hatari kubwa ya kupata pumu kwa kuwa watu wengi wenye msongo wa mawazo hujaribu kujituliza kwa kutumia vileo na kuvuta tumbaku hivyo kuongeza uwezekano wa kupata pumu. Ingawa utafiti wa hivi karibuni umegundua mfumo wa kingamwili hubadirika kutokana na msongo wa mawazo (Stress) kitu kinachoweza kusababisha kutengenezwa kwa kingamwili (Antibodies) za igE zinazosababisha pumu.
Chembe za urithi pia huhusianishwa na ugonjwa wa pumu. Kuna chembe za urithi 100 zinazohusianishwa na pumu. Uwezekano wa kupata pumu kutokana na lurithi kwa wazazi ni 3 ya 5. Taasisi za kudhibiti magonjwa ya Marekani (The Centers for Disease Control USA) zinasema kuwa na wazazi wenye pumu huongeza hatari ya mtoto kupata pumu pia mara 3 hadi 6.
Tatizo la ngozi linalosababishwa na mzio/allergy (Eczema/Atopic dermatitis). Watoto 40% hadi 50% wenye tatizo hili hupatwa na pumu na inawezekana wenye tatizo hili hubanwa na pumu ya mara kwa mara.
DALILI ZA PUMU
Sio watu wote wenye pumu huwa na dalili hizi. Vilevile kuwa na dalili hizi hakumaanishi una ugonjwa wa pumu.
=> Kukohoa. Kikohozi kinachotokana na pumu huwa kinakuwa kikali sana hasa wakati wa usoku au asubuhi sana.
=> Kutoa sauti kama filimbi au mluzi wakati wa kupumua.
=> Kubanwa kifua. Mgonjwa huhisi kama kifua kinabanwa na kitu au kuna kitu kizito kimewekwa juu ya kifua.
=>Kupungukiwa na pumzi. Wagonjwa wenye pumu huhisi pumzi imekosekana, zaidi inakuwa ni ngumu kutoa pumzi kutoka katika mapafu.=
JINSI YA KUTIBU & KUDHIBITI PUMU
Pumu ni ugonjwa sugu usiotibika ila unaweza kudhinitiwa. Ili kudhibiti ugonjwa huu, uhusiano mzuri kati ya mgonjwa na daktari unahitajika sana.
Ili kudhibiti yafuatayo huhusishwa :-
=> Kuzuia dalili hatari kama kukohoa na kupungukiwa na pumzi.
=> Kupunguza uhitaji wa dawa za kutuliza maumivu haraka kama Aspirin
=> Kufanya kazi kwa kiasi na kulala vizuri wakati wa usiku.

- See more at: http://www.fikrapevu.com/mambo-muhimu-ya-kufahamu-juu-ya-pumu-asthma-na-matibabu-yake/#sthash.LMU827X6.dpuf

  •  
    Support : Blog designer | Blogger | Developer | | KakyteeMedia.InC
    Copyright © 2011. Kakytee.com - All Rights Reserved
    Template Modified by KakyteeMedia
    Proudly powered by Blogger