Headlines News :

Tuesday, October 22, 2013

MAMBO 20 YA KUFANYA UHUSIANO WENU UBAKI KWENYE FURAHA SIKU ZOTE

  1. FANYA UCHAGUZI SAHIHI

Hapa ndipo watu wanapotakiwa kutumia akili zao mpaka zile za akiba, ukikosea hapa ni rahisi sana kuvurunda hapo baadaye. Uhusiano wenye nguvu, hujengwa na penzi la kweli. Acha kukurupuka, lazima ujihakikishie kwamba uliyenaye ni chaguo kutoka ndani ya moyo wako.
Najua una maswali; kwamba utawezaje kumjua mwenye mapenzi ya kweli, hiyo ni mada ambayo nimeshaandika mara kadhaa katika ukurasa huu na gazeti damu na hili, Ijumaa. Kimsingi, kwa kufuata maelekezo hayo, mwenzi ambaye unatarajia kuwa naye katika maisha ya ndoa hapo baadaye, lazima msingi uwe ni uchaguzi sahihi.
Sikia, watu wengi waliokuwa na fedha, wamefilisika baada ya kuoa/kuoleawa na wenzi ambao si sahihi. Aidha, wapo wenye mafanikio makubwa sana, ambayo wameyapata baada ya kuoa/kuolewa na wenzi sahihi. Rafiki zangu, si jambo rahisi kumpata yule aliye sahihi. Inahitaji utulivu.
Yapo mengi sana ambayo unapaswa kuyaangalia, ambayo nimekwishaeleza sana katika makala zangu zilizopita. Wakati nahitimisha kipengele hiki, shika neno moja tu; unapomchagua mwenzi wa maisha yako, hakikisha ni yule aliye sahihi! Tuendelee na kipengele kingine.
 
2. JIELEZE
Migogoro mingi baina ya walio kwenye uhusiano husababishwa na wenzi kutowafahamu vyema wenzao. Usiingie katika mkumbo huu, ni suala la kujieleza tu. Kumweleza mpenzi wako ulivyo, kutamfanya ajue vitu unavyopenda na usivyopenda. Aidha, kama unao udhaifu wowote wa kiafya na kadhalika, mweleze mwenzako.
Kumweleza kutamfanya ajiamini kuwa anapendwa. Kunaonesha unavyojiamini na unayetaka mwenzako ashirikiane na wewe katika hali uliyonayo. Si vibaya mwenzio kukufahamu kwamba una hasira sana. Yes! Maana akishajua hilo, ataacha utani unaokaribia kukuudhi maana anajua vizuri kuwa una hasira za karibu.
Ipo mifano mingi sana, lakini kikubwa cha kushika katika kipengele hiki ni kuwa mkweli kwa mwenzako kuhusu maisha yako. Acha kumdanganya kwamba familia yenu ina uwezo mkubwa, wakati ni wa kawaida. Kuwa mkweli, mapenzi si utajiri, ni hazina iliyojificha ndani ya moyo.
Kama anakupenda, anakupenda tu! Siku akigundua kwamba unamdanganya, pendo lake litapungua kwa kiasi kikubwa sana. Jieleze kwa uwazi na ukweli kutoka ndani ya moyo wako. Naye atakuheshimu na utakuwa umetengeneza mwanzo mzuri wa kuelekea kwenye ndoa isiyo na migogoro.
3. MPE UHURU
Wengi wanaamini kumbana mpenzi ni njia sahihi ya kumfanya awe mwaminifu, si kweli. Kuna wenye tabia ya kuvizia simu za wenzao na kuzipekua, si utaratibu mzuri. Mpe uhuru, usimbane! Kuonesha kumwamini sana mpenzi wako, kunamfanya naye aishi ndani ya uaminifu.
Kumchunga hakumnyimi kuendelea na mambo yake, sana sana atafanya kwa siri kubwa. Kumpa uhuru, kutamwogopesha, atajua yupo na mwaminifu ndiyo maana hafuatiliwi, hapo utakuwa umechochea naye awe mwaminifu kama wewe.
 
4. ACHA PAPARA
Katika hatua za mwanzo kabisa za uhusiano wenu, hutakiwi kuwa na papara katika jambo lolote. Kila kitu kifanywe kwa utaratibu. Huna sababu ya kurukia mambo, hasa makubwa.
Wengi wamekuwa na haraka sana ya kukutana kimwili, haya ni makosa makubwa sana. Haraka ya nini kama unatarajia awe wako wa maisha. Ngoja nikuambie rafiki yangu, unapoanza kuulizia mapema mambo ya faragha, unamfanya mwenzako ashindwe kukuamini.
Kwanza, atahisi wewe upo kwa ajili ya kutaka kujistarehesha tu, lakini pia anaweza kufikiria kwamba unapenda sana mambo ya chumbani. Kumfanya agundue kasoro hiyo ni tatizo kubwa sana kwako.
Hata hapo baadaye mtakapoingia kwenye ndoa, ni rahisi zaidi kukumbuka mambo ya zamani, kwamba yupo na mtu anayependa sana mambo ya mahaba. Kwa maneno mengine, hata akihisi tu au kusikia kwamba una mtu mwingine pembeni, atapeleka moja kwa moja hisia zake kwenye kuamini moja kwa moja juu ya jambo hilo.
Papara si jambo jema kabisa kwa mwenzi ambaye unatarajia awe wako wa maisha. Tulia, mchunguze kwanza. Kumbuka unatakiwa kufikiria kuhusu mustakabali wa maisha yako ya baadaye, kama ndivyo, huna haja ya kuharakisha mambo ya mapenzi.
5. JENGA URAFIKI
Ukitaka kutengeneza uhusiano wenye nguvu, basi zingatia zaidi urafiki. Kumfanya mwezi wako rafiki ni silaha kubwa na yenye nguvu katika kuuimarisha uhusiano.
Mwenzi wako anapojiona kama rafiki, anakuwa katika nafasi nzuri ya kuzungumza chochote, ikiwemo matatizo na migongano mbalimbali kama rafiki zaidi.
Hawezi kukuficha siri zake. Atakuwa na wewe muda wote na atakusogeza karibu yake kwa kila kitu. Hata penzi lenu pia litakuwa na nguvu zaidi. Urafiki ni kila kitu ndugu zangu.
Acha tabia ya kumkaripia mpenzi wako, jenga mazoea ya kujadiliana zaidi kuliko kutumia kauli za ukali. Rafiki zangu, yote hayo niliyoyazungumza yanajengwa na jambo moja tu; urafiki!
 


















6. MSIFIE
Wengine wanaweza kushangazwa na kauli hiyo, lakini nataka kuwaambia kuwa kati ya mambo muhimu kabisa kumfanyia mpenzi wako na kulifanya penzi kuwa jipya ni kumsifia. Unapomwambia mwenzako kauli nzuri za kumbembeleza kuwa yeye ni mzuri, anakuvutia kwa kila hali, unajenga penzi.
Unamfanya anajihisi wa thamani, atajiamini kuwa yeye ni mkamilifu, si kwa watu wanaomzunguka pekee, bali hata wewe ambaye umemchagua na kumfanya awe wako.
Kama huna utamaduni wa kumsifia mpenzi wako, huu ni wakati wako wa kufanya hivyo kwa lengo la kuzidisha mapenzi na kuyapa nguvu.
 
7. SAIDIA KUKUZA UHUSIANO WENU
Kila mmoja ana wajibu wa kuhakikisha penzi linazidi kukua siku hadi siku. Kwa maana hiyo, wewe kwa nafasi yako unatakiwa kuhakikisha unakuwa mstari wa mbele kukuza uhusiano wenu.
Kuna mambo mengi sana ambayo yakifanyika, yanakuza uhusiano. Vipo vitu vya kufanya, kutoka pamoja ni njia mojawapo ya kukuza uhusiano. Rafiki zangu, mnapokwenda katika matembezi, husaidia kubadilisha mapenzi na kuonekana mapya.
Si lazima kwenda nje ya mji, kikubwa ni kuzingatia mfuko wako. Hata mkienda mahali pa kawaida tu, mkanywa juice na keki, bado ni nafasi nzuri kwenu ya kukuza uhusiano huo.
Kila mmoja ana wajibu wa kufanya hivyo, lakini hutakiwi kumsubiri mwenzako afanye, wewe kwa nafasi yako unatakiwa kuhakikisha unamfanya mwenzi wako afurahie uhusiano wenu. Kufanya hivyo, kutampa deni na yeye la kufanya hivyo kwako.

8. MFANYE NAMBA MOJA
Kuna baadhi ya marafiki wana fikra potofu (hasa wanaume). Hawa wanaamini kumpa mwanamke nafasi katika maisha ni kumfanya akukalie. Si kweli. Mwanamke unapompa nafasi ya kwanza, anaufurahia uhusiano wenu.
Anajiona mwenye hadhi kubwa zaidi kwako, hutafuta njia za kukufanya umpende maradufu, kuliko kumuacha akijiona hana nafasi.
Ongozana na mpenzi wako kwenye kumbi za burudani, mialiko ya sherehe mbalimbali, lakini pia mpe kipaumbele kwa kila kitu. Hili halihitaji elimu ya darasani. Chunguza wenzako wanaowapa wenzi wao kipaumbele wanavyoishi.
Achana na mifumo ya kizamani, ukimpa mwenzako usawa anajiona ana nafasi kwako na thamani katika uhusiano mlionao.
 
9. MPE NAFASI
Hapa hakuna kitu kikubwa sana, ni kiasi cha kumpa nafasi katika mambo yako muhimu. Mathalan unataka kununua kiwanja Gongo la Mboto; Hata kama umeshaweka kila kitu sawa, lakini kumshirikisha tu, kutamfanya ajione mwenye nafasi kubwa kwako.
Hili si kwa wanaume pekee, hata wanawake nao wanapaswa kutoa vipaumbele kwa wanaume zao. Hii itasaidia kwa kiasi kikubwa sana kuongeza ladha ya mapenzi kwa wapendanao.
Inawezekana elimu hii imekupitia kushoto, hebu jaribu uone mafanikio yake.
Kumpa nafasi mwenzako katika mambo yako, tafsiri yake ni kumuamini na kumfanya azidi kujiamini kwako. Ni rahisi sana, lakini habari njema kwako ni kwamba, atakusikiliza kwa kila kitu, maana anajiona yeye ni sehemu yako kikamilifu.
 
10. MTAMBULISHE
Mapenzi ya siri yana ukomo wake marafiki zangu. Ngoja niwaambie, unapokuwa unapenda mapenzi ya siri sana, unampa wakati mgumu mwenzako.
Ni rahisi kufikiria kwamba, unafanya hivyo kwa kuwa ama hujiamini au una mtu mwingine. Weka mambo hadharani. Mtambulishe mwenzi wako kwa marafiki zako.
Jiamini, unapokutana na mtu uliyesoma naye zamani au kuishi naye sehemu moja, mwambie kwamba uliyenaye ni mwenzako na unatarajia kuingia naye kwenye ndoa.
Kufichaficha kunaondoa utamu wa mapenzi. Kunazidisha maswali ambayo hayana majibu. Kama yapo ni huyo mwenzako kujijibu mwenyewe. Kwa kawaida, hatajipa majibu mazuri.
Yatakuwa ya kinyume – yenye tafsiri mbaya. Kwamba yawezekana hutaki kumtambulisha kwa kuwa una mtu mwingine. Je, ni kweli? Kama ndivyo huna sababu ya kumpotezea muda mwenzako. Kama si kweli, basi amka. Gundua kwamba ulikuwa unafanya makosa na uanze ukurasa mpya.
 
11. GUSIA MAMBO YA KIIMANI
Kuzungumzia mambo ya dini kulingana na imani yenu, kutamsogeza mwenzako kwenye ukweli kuwa una lengo naye la kuungana katika maisha ya ndoa. Angalizo kwako ni kwamba, wakati unamweleza hayo, iwe kweli yanatoka ndani ya moyo wako. 

 12. WAHUSISHE VIONGOZI WA DINI
Ikiwa uhusiano wenu umekomaa, unatakiwa kuwashirikisha viongozi wa dini. Angalia mazingira, unaweza kwenda naye, au kwenda mwenyewe na kuwaeleza nia yako. Waambie wakuombee au wawaombee ili uhusiano wenu uwe na nguvu.
Kumbuka ndoa ni tendo la heri, hivyo shetani naye hutumia nafasi hiyo kuwaharibia! Kumuingiza Mungu katika uhusiano wenu kuna maana, mtakuwa katika ulinzi wenye nguvu zaidi.
Yamkini pia, kama uliyenaye si chaguo kutoka kwa Muumba atamuengua mikononi mwako na kukupeleka palipo sahihi. Usiogope, nenda kaonane na viongozi wa dini na uwaeleze kinagaubaga.
 
13. KAMILISHA TARATIBU ZA KIFAMILIA/KIMILA
Ikiwa una uhakika kuwa mwenzako ndiye uliyemkusudia (zaidi kwa wanaume) wajulishe wazazi wako, kisha anza taratibu za kimila na kifamilia. Tuma wazee wapeleke posa, lipa mahari, halafu sasa anza kutimiza maagizo mengine yote utakayoagizwa.
Ni njia ya kuelekea kwenye ndoa. Uhusiano wenye baraka za wazazi, si tu kwamba unakuwa na nguvu, bali una radhi za wazazi wenu wa pande zote mbili. Je, kwa hali hiyo uhusiano wenu hautaimarika? Bila shaka utazidi kuchanua.

14. JADILINI KUHUSU NDOA
Hii ni hatua ya muhimu kabisa katika kuelekea kwenye ndoa. Mnapaswa kuijadili ndoa yenu ni ya namna gani? Kama imani zenu zimetofautiana, nini kifanyike? Pindi mtakapojadiliana, mtaweza kupata muafaka juu ya ndoa ambayo ni sahihi kwenu.
Ndugu yangu, usilazimishe kumbadilisha mwenzako akufuate katika imani yako kama yeye hataki au pengine kuna vipingamizi katika familia yao. Kila mmoja wenu anapaswa kuweka hoja mezani na mnazijadili kwa mapana yake na mwisho muafaka utapatikana, mtaoana.
Hakuna kinachoshindikana katika majadiliano, tumia lugha nzuri kumshauri mwenzako ili ajue unamjali hivyo ni rahisi kuridhia ulichomshauri. Ieleweke tu ndoa yoyote mtakayokubaliana kupitia majadiliano yenu, basi itadumu kuliko mkitumia njia ya kulazimishana.
(b) Kwa wanandoa hapa sasa mnisome kwa makini maana wengi wamekuwa wakifeli katika hatua hii kutokana na kujisahau. Mikikimikiki ya maisha inapoibuka inaweza kuwafanya kila mmoja wenu akawa na maamuzi yake katika maisha hata kama mwanzoni (kabla ya ndoa) dhamira yenu ilikuwa njema.
Siku ya leo, Lets Talk About Love itakumegea vipengele sita ambavyo kimsingi ukivisoma kwa makini itakuwa ni dozi sahihi kama mwanandoa kuweza kujua siri hizi muhimu za kufurahia mapenzi yenu na nikushauri kuitumia kila siku.
15. WEKENI MIPANGO PAMOJA
Wanandoa wengi wamekuwa wakijisahau pindi wanapokuwa ndani ya ndoa. Inawezekana awali walikuwa na mikakati mizuri lakini baadaye mmoja wao huanza kujiamulia bila kumshirikisha mwenzake. Tatizo hili lipo zaidi kwa wanaume, mfumo dume unachukua mkondo wake. Utakuta mwanaume anafanya maamuzi peke yake akiamini yeye ndiyo kila kitu.
Jeuri hii inakuja hasa pale mwanaume anapoamini kuwa yeye ndiyo chanzo cha fedha wanayotaka kufanyia kitu fulani. Ataamua bila kumshirikisha mkewe kwa kuwa fedha anakuwa nazo yeye bila kujua mipango yote inapaswa kuzungumzwa pamoja kabla ya kufanya maamuzi.
Ndoa ni makubaliano baina ya watu wawili hivyo basi, katika kila jambo la maendeleo litafanikiwa pale tu mtakapolipanga pamoja. Ndugu yangu, acha kujiona wewe ni zaidi katika ndoa kutokana na kipato ulichonacho. Fedha si lolote si chochote katika maisha ya ndoa. Fedha zisibadilishe maamuzi ya mipango yenu, kila mnachotaka kukifanya basi mkifanye pamoja.
16. TUMIA MAJADILIANO ZAIDI
Yamkini wote wawili mlifanya majadiliano kabla ya kufikia maamuzi ya ndoa, basi ni wajibu wenu kuishi katika majadiliano kila siku. Wapo watu wasiopenda kuona ndoa za watu zinakuwa na furaha. Wataingilia na kuwafanya mgombane. Inawezekana pia mkapishana kauli katika mazungumzo, busara huhitajika.
Kutofautiana kwa kauli pamoja na vitu vingine, vinaweza kumalizwa kwa njia ya majadiliano. Jadilini katika lugha nzuri itakayomfanya mwenzio aone thamani yake.
Mkijadili yote kwa uyakinifu, mwisho mtagundua kumbe kilichokuwa kinawatatiza ni kitu kidogo ambacho hakikuhitaji nguvu kubwa kukitatua. Mnapojadiliana ni rahisi pia kutambua kosa lilikuwa wapi au lilisababishwa na nani, hivyo ni rahisi kumuepuka. 

  17. PALIZI YA NDOA
Kama ilivyo kwa mazao yakiwa shambani yanavyohitaji kupaliliwa ili yaweze kushamiri, vivyo hivyo katika ndoa. Ndoa inapaswa kupaliliwa kila siku. Jaribu kila wakati kusoma alama za nyakati, vitu gani anavipenda mwenzako basi umfanyie kila wakati.
Mfano unaweza kupanga siku moja katika wiki ukamchukua mkeo au mumeo na kumtoa nje kimatembezi. Ndoa hupaliliwa na vitu kama hivyo. Zawadi za hapa na pale zisipungue, acha kuishi kwa mazoea eti kwa kuwa tayari ni mkeo au tayari ni mumeo.
Unapoipalilia ndoa katika staili za zawadi, mitoko na vitu vingine huifanya ionekane mpya kila siku. Mnunulie mkeo au mumeo vazi unaloona linaendana na wakati mlionao.

18. KINYWA CHENYE LADHA
Inawezekana ukaona labda nazungumzia kitu cha kawaida sana, lakini kama ukitafakari kwa kina na kwa mapana yake, utagundua kwamba ni mjadala wenye maana katika ndoa.
Hata kwenye Kitchen Party, sherehe za ndoa n.k, suala la kinywa chenye ladha nzuri huzungumzwa sana, ila hapa nitakuongezea baadhi ya vitu vingine usivyovijua.
Kwa kawaida, wanawake ndiyo ambao huaswa zaidi katika kuwa na kauli nzuri kwa waume zao. Wanaume wamesahaulika kabisa. Wanaonekana kama wao hawana wajibu wa kuwa na kauli nzuri kwa wake zao; jambo hili si la kweli hata kidogo.
Wote wanapaswa kuweka masikilizano kwa kauli ya pamoja, huku kila mmoja akiwa na shabaha ya kuhakikisha mwenzake haudhiki na maneno yake. Ni jambo jepesi sana – kuwa na ulimi wenye ladha.
KUJITAMBUA kwamba unayezungumza naye ni mke/mumeo. Hebu jiulize, ikiwa mwanzoni wakati wa uchumba wenu mliweza kuwa na kauli nzuri, kila mmoja akiwa na hamu ya kumsikiliza mwenzake muda wote, iweje katika ndoa?
Jibu la swali hili litakuwa mwongozo mzuri zaidi wa kuinakshi ndoa yenu kuwa bora yenye furaha siku zote. Ndugu zangu, furaha ndiyo kila kitu katika uhusiano wowote ule. Kukiwa na furaha, hakuwezi kuingia tatizo lolote. Litapitia wapi, wakati mioyo ina amani?
Ikiwa kinyume chake, ni rahisi hata kugombana, maana hata mgombanishi hupata nafasi zaidi sehemu isiyo na amani, isiyo na majadiliano, pasipo na maelewano. Usikubali kuwa katika ndoa ya namna hiyo.
 
19. EPUKA MANENO YA KUUDHI
Kipengele hiki hakina tofauti sana na kilichopita, lakini hapa kuna la zaidi la kuongezea. Kuna wakati wenzi wanaweza kuingia katika mtafaruku ambao chanzo chake ni cha ajabu kabisa! Kwa mfano, unakuta mpenzi anamwambia mwenzake: “Mh! Na wewe unanuka sana mdomo!”
Kauli gani hiyo kwa mpenzi wako? Mwanaume unalala naye kila siku, kwa nini umwambie ananuka? Wewe ukifanya hivyo, huko nje wamuambieje? Kwanza kama ni kweli ana tatizo hilo, ni jukumu lako kumtibu, lakini pia kumtunzia siri.
Kama nje anachekwa, ndani ya familia pia anachekwa, wapi atapata faraja? Yapo maneno mengi sana yenye kuudhi, lakini hapa nitataja machache. Wengine wanawaambia wenzao wananuka kikwapa, hawajapendeza, hawana akili nk.
Haya ni maneno ya kuudhi. Hebu fikiria kauli kama hii mtu anamtamkia mkewe! “Yaani kweli wewe huna akili, kitu kidogo kama hicho kweli unaweza kukosea? Ndiyo maana wenzetu wanafanikiwa kimaisha, wanatuacha. Sijui nilikutana na wewe wapi?...maisha yangu yanazidi kuwa giza tu, nikiwa na wewe!”
Acha maneno ya kufuru, kwani siku zote hukuona upungufu wake? Kuwa makini na kauli zako. Ndoa yako utaivunja wewe mwenyewe, pia kama ni kuijenga, utaijenga wewe mwenyewe!
 
20. UBORA KATIKA TENDO LA NDOA
Hapa ndipo panapotakiwa kupewa heshima kubwa zaidi kuliko vipengele vyote vilivyotangulia. Katika masomo yaliyopita, nimewahi kufafanua hili kwa undani zaidi, leo nitagusia juu juu tu!
Rafiki zangu, tendo la ndoa ni la heshima. Halitaki papara na linatakiwa kupewa nafasi na kila mmoja kuridhika. Acha kujifikiria mwenyewe, maana hapa ndipo panapopatikana mianya ya kutoka nje ya ndoa.
Hakikisha mwenzako anaridhishwa na wewe mnapokuwa chumbani. Tafuta elimu zaidi ya kufurahia tendo hilo ili mwenzako awe na sababu ya kuwa na wewe. Sikia nikuambie, tendo la ndoa kwa wanandoa hasa waliozoeana linachosha!
Huu ni ukweli ambao wengi wanaupinga. Yes! Linachosha na kukikanaisha. Hakuna kipya. Mwanaume yule yule. Kitanda kile kile, chumba kile kile. Lazima umchoke.
Hata hivyo, ukiwa mbunifu utaendelea kumuona mwenzako mpya kila siku. Badilisheni mazingira, tafuteni muda wa kutoka pamoja angalau mara moja ndani ya miezi mitatu – kwa mwaka mara nne.
Yapo mengi sana, elimu hii ni pana, hasa kama utakuwa mbunifu na mwenye kuisaka kila siku. Rafiki zangu, nadhani mnafahamu namna inavyokuwa vigumu kueleza kila kitu hapa gazetini, lakini kikubwa cha kumalizia mada hii ni hiki; unapokuwa na mwenzako faragha, ujue kuwa anategemea zaidi wewe kumfanya afurahie tendo hilo.
Ukijua hivyo, naye akajua hivyo, furaha ya tendo la ndoa itadumu siku zote za ndoa yenu.

Use Facebook to Comment on this Post

  •  
    Support : Blog designer | Blogger | Developer | | KakyteeMedia.InC
    Copyright © 2011. Kakytee.com - All Rights Reserved
    Template Modified by KakyteeMedia
    Proudly powered by Blogger